na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu – Waefeso 4: 23
Neno la Mungu linatuasa, kwani Roho Mtakatifu anafahamu jinsi ilivyo rahisi kwetu kujikuta tunaufuatisha mfumo wa dunia hii katika namna tunavyoishi, jambo ambalo litatusababisha tukose kuyafahamu mapenzi ya Mungu na kujikuta tunaishi maisha yasiyompendeza wala kumtukuza Mungu.
Neno la Mungu lina uweza wa kutubadilisha nia zetu ili ziendane na maandiko yanavyosema na hivyo kutuwezesha kutembea kwa ushindi katika maisha yetu. Tunapolisoma, tunapolitafakari na tunapolitii Neno, nia zetu na hata utendaji wetu unabadilika katika eneo husika, kuendana na Neno lisemavyo.
Tusifuatishe namna ya dunia hii, yaani badala ya kuchukulia mambo kama wasiomjua Mungu wanavyofanya, tunapaswa kusimama na Neno linavyosema. Tuhakikishe kuwa Neno la Mungu linajaa kwa wingi ndani yetu katika hekima yote, tulisome, tulitafakari na tulitii Neno.
Matokeo yake badala ya kukiri udhaifu ama kushindwa, tutakiri Neno linavyosema “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu”. Tunapokabiliana na changamoto za kiuchumi, badala ya kukiri “Nimechacha!” au “Nimekwisha!” tutakiri “Bwana ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu”. Badala ya kusema “Naogopa”, tutasema “Bwana ni ngome yangu, kimbilio langu, nimwogope nani?” Na matokeo yake tutauona mkono wa Bwana ukitupigania katika yote kwa ajili ya utukufu wake.
Bila shaka umeweza kupata picha kidogo ya jinsi Neno linavyoweza kutubadlisha na jinsi ambavyo Mungu anaweza kujitwalia sifa na utukufu katika maisha yetu.
Tunapojizoeza kusimama na Neno linavyosema inakuwa ni rahisi kuyajua mapenzi ya Mungu katika yale tunayokabiliana nayo na hivyo kuweza kutenda yale yatupasayo.