14 Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; 15 mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo. – Waebrania 12:14-15 SUV
Neno la Mungu linatuhimiza kutafuta kuwa na amani na watu wote kwa bidii tena bila kubagua, maana tukiishi kwa amani na wote wanaotuzunguka tutaweza kuwavuta kwa ushuhuda wa maisha yetu kwani sisi ni barua ya wazi inayosomwa na wote. Lengo kuu mojawapo la kuishi kwa amani na wote ni ili nao wapate fursa ya kuisikia Injili na kuokolewa, kwa maana tukiishi na majirani zetu kiugomvi ugomvi, kiukorofi ukorofi tutakosa ujasiri wa kuwashuhudia, licha ya kwamba tutawafanya waifunge mioyo yao washindwe kuipokea Injili toka kwetu.
Yatupasa kuishi maisha ya utakatifu. Utakatifu wa Mungu hatuupati kwa kujitahidi kwa juhudi zetu kuzishika zile amri kumi, la hasha. Katika zama hizi za Agano Jipya, baada ya Bwana Yesu kukamilisha kazi ya kutukomboa na kutupatanisha na Mungu, tunavikwa utakatifu na Mungu mwenyewe kwa Neema yake tunapomwamini Bwana Yesu kama Bwana na mwokozi wetu. Roho wa Mungu ndani yetu anatuongoza katika njia za Haki kwa ajili ya jina lake, anaiandika sheria yake mpya ndani yetu, sheria ya Roho wa Uzima (Romans 8:2) na amri mpya ya Upendo (Yohana 13:34, 1 Yohana 4:19 -21). Utakatifu tunaupata toka kwa Kristo mwenyewe, kwani yeye alifanyika kuwa dhambi ili sisi tuweze kufanyika kuwa Haki ya Mungu (2 Wakorintho 5:21). Ndani yake sisi tunafanyika kuwa wana wa Mungu, watakatifu, watu waliotengwa mahususi kwa ajili yake ili tupate kuzitangaza sifa zake. Utakatifu ulioko ndani yetu utadhihirika katika mienendo yetu iliyojaa upendo, furaha na amani katika Roho Mtakatifu, na wale wasiomjua Mungu wataweza kumwona na kumfahamu kupitia sisi.
Kuishi kwa amani na wote na kuwa na utakatifu vinawezekana pale tu tutakapohakikisha kuwa hatuipungukii Neema ya Mungu. Neema ya Mungu ni fadhila zake na wema wake ambao hatuustahili ila anatukirimia bila kikomo kwa sababu ya kazi kamilifu ya ukombozi aliyoifanya Bwana Yesu kwa kufa na kufufuka kwake. Katika Kristo tuna haki zote mbele za Mungu kama watoto wake wapendwa, tunao ujasiri wa kwenda mbele zake bila hofu, kwani dhambi zetu zilizotutenganisha naye Bwana Yesu alishazichukua zote katika mwili wake juu ya msalaba. Kwa hiyo leo hii vyote tunavyopokea maishani mwetu tukiwa ndani ya Kristo ni kwa Neema yake, siyo kwa jitihada zetu.
Tunapojaribu kupokea chochote toka kwa Baba kwa jitihada zetu wenyewe tukidhani zitatustahilisha mbele zake tunaipungukia Neema ya Mungu na matokeo yake shina la uchungu linaanza kuchipuka ndani yetu, hasa pale tuwaonapo wengine wakibarikiwa na kufanikiwa “kirahisi tu” bila kufunga sana na kukesha sana wakiomba sana kama sisi. Tafadhali nielewe, kufunga, kukesha na kuomba kuna nafasi yake, lakini kamwe siyo vigezo vya kutustahilisha kupokea chochote toka kwa Mungu leo hii. Vyote tunavyovihitaji kwa ajili ya maisha haya na utauwa leo hii viko ndani ya Kristo na tunavipata kwa kuzidi kumjua sana yeye aliyetuita kwa utukufu na wema wake (2 Petro 1:3). Ahadi zote za Mungu kwetu sisi tulio katika Kristo ni ndio nasi tunasema amina na kuzipokea!
Wapendwa tusiipungukie Neema ya Mungu na kuruhusu shina la uchungu lichipuke na kututia unajisi sisi wenyewe na wale wanaotuzunguka, na kama tunajikuta na hatia katika eneo hilo tusikubali adui atutese kwa kutujazia shutuma na hukumu tujione hatufai. Neno linasema ikiwa mioyo yetu inatuhukumu yeye ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote kwa hiyo basi tusiendelee kulea shina la uchungu mioyoni mwetu tutubu kwa kukiendea Kiti cha Rehema ili tupate Neema na Rehema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. Mbarikiwe!
Kumbuka ya kuwa Baba yako wa mbinguni anakupenda sana na hataki ukose kupokea,kushiriki na kufurahia vyote alivyo navyo kwa ajili yako. Anayo makusudi mema na maisha yako. Mpendwa, Mungu yuko upande wako, hayuko kinyume nawe ndio maana anakuasa na kukutia moyo usiipungukie Neema yake. Kwa imani pokea wingi wa Neema na kipawa cha Haki upate kutawala pamoja Kristo (Warumi 5:17)
Mungu na azidi kuwabariki,
Patrick
Filed under: NENO
